Kesi ya Ahera
by J.M. Manoah
Kesi ya Ahera ni hadithi kumhusu Daktari Richard Pingo aliyepatikana ameuawa kinyama mtaani Ronda, mjini Dunga; katika Jamhuri ya Bugasi. Mkewe, Dibla, anapoenda kuripoti kifo cha mumewe katika kampuni ya maziwa ambako Daktari Pingo alikuwa akifanya kazi, anapata kuwa jina la mke wa Daktari Pingo katika faili za kampuni hiyo ni Lena Kisai wala si lake, Dibla.
Maji yanazidi unga Dibla anapoukosa mwili wa mumewe katika mochari ulimokuwa umehifadhiwa. Kunazuka kukurukakara kati ya Dibla na Lena huku wote wawili wakiung'ang'ania mwili wa Daktari Pingo. Je, kwa nini Daktari Pingo aliuawa? Je, Dibla atafaulu kuuzika mwili wa mume wake? Ni nani ndiye mke wa halali wa Daktari Pingo? Kisa hiki ni kimoja tu kati ya vingine vingi katika jamhuri ya Bugasi.
Bwana James M. Manoah ni malenga mkongwe aliyeshiriki utunzi wa mashairi yaliyochapishwa katika gazeti la Taifa Leo, kwa jina la lakabu, Mwana Yatima. Ana kipawa cha kipekee katika kusuka hadithi za Kiswahili.